NEWZ:Mwenyekiti Barclays ajiuzulu



Marcus Agius aliamua binafsi kujiuzulu kutokana kwa kile alichotaja katika taarifa yake ya kujiuzulu kama pigo kubwa linalotokana na kuharibiwa sifa kwa kampuni hiyo kwa sababu ya madai ya kuwalaghai wateja kupitia nyongeza haramu ya riba.

Wito umetolewa kuwa afisa mkuu mwandamizi wa kampuni hiyo, Bob Diamond ajiuzulu, kwa sababu alikuwa akisimamia uwekezaji wa benki hiyo wakati mpango ulipofanywa kulaghai wateja kupitia kwa riba inayotozwa katika benki hiyo.
Hata hivyo wakurugenzi wa Barclays wameamua kuwa Bwana Diamond ataendelea kufanya kazi.
Kwa hivyo Bwana Agius, ambaye pia ni mwanachama wa Bodi, aliamua, huku akiungwa mkono na wenzake, kujitwika lawama zote zinazotokana na madhambi yanayokabili Benki ya Barclays na hasira yote waliyo nayo wenye hisa wa benki hiyo.

Mtu anayetazamiwa kuchukua mahali pake ni mkurugenzi mwingine, Sir Mike Rake, ambaye kwa sasa atalazimika kujiuzulu vyeo vyake vya kuwa mwenyekiti wa Easyjet na BT.
Naye Bwana Diamond hajajiondoa katika lawama bado kwani atahojiwa na Wabunge kuhusu mawasiliano ya siri ya mwaka wa 2008 kati yake na naibu wa Gavana wa Benki Kuu, Paul Tucker.

Meneja wa Barclays wanaamini kuwa ni katika mawasiliano hayo ambapo Benki Kuu ya Uingereza iliamuru Benki hiyo kudanganya kuhusiana na riba inayotozwa.

Hiyo haikuwa kweli lakini Bwana Diamond atalazimika kuwaeleza Wabunge anachokumbuka Bwana Tucker akimweleza wakati ule na kile ambacho baadaye aliwaeleza wafanyakazi wenzake.
Itakuwa aibu kubwa kwao iwapo yeye au Bwana Tucker watagunguliwa kwamba waliwashawishi wenzao kulaghai kupitia riba haramu.

No comments:

Post a Comment